HALMASHAURI YAKOPESHA VIKUNDI 16 VYA KATA YA KINDAI MANISPAA YA SINGIDA

Na Jumbe Ismailly SINGIDA  

 


HALMASHAURI ya Manispaa ya Singida imetoa mikopo kwa vikundi 16 vya wanawake pamoja na vijana katika kata ya Kindai yenye thamani ya shilingi milioni 68,500,000/= ili kuviwezesha vikundi hivyo kukuza uchumi na kujiongezea kipato katika kipindi cha kuanzia mwaka 2020 hadi mwaka 2025.

 

Diwani wa Kata ya Kindai,katika Halmashauri ya Manispaa ya Singida,Omari Salumu maarufu kwa jina la Kinyeto aliyasema hayo kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika katika mtaa wa Kibaoni alipokuwa akitoa taarifa ya utekelezaji wa ilani ya uchaguzi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM).

 

Aidha diwani Kinyeto hata hivyo alifafanua kwamba kati ya kiasi hicho cha fedha,shilingi milioni 55,500,000/= zilitolewa mikopo kwa vikundi 16 vya wanawake na vijana kwa kipindi cha mwaka 2020 hadi juni,mwaka 2024 na shilingi milioni 13 zilitolewa mikopo kwa vikundi vitatu vya wanawake kuanzia mwezi julai,mwaka jana hadi mwezi Aprili mwaka huu.

 

“Hizo ndio fedha taslimu ambazo zimeletwa katika Kata ya Kindai na vikundi hivyo vyote vimepewa na vingine vyote vimeweza kurejesha na bado kuna vikundi vichache havikuweza kurejesha,lakini pia baada ya serikali kufanya mabadiliko ya muundo mzima wa utoaji wa fedha za mikopo vikundi vitatu vimeweza kukidhi vigezo na vimeweza kupewa fedha na jumla ya fedha iliyoweza kutolewa ni shilingi milioni 13”alifafanua diwani huyo.

 


Hata hivyo Kinyeto aliweka bayana kuwa kutokana na mabadiliko ya utoaji wa mikopo hiyo kufanyika hivyo aliwataka wanawake vijana na watu wenye ulemavu kwenda kwa maafisa watendaji wa kata kwa ajili ya kupatiwa maelekezo ya taratibu ambazo zinaweza kukidhi vigezo vya kupatiwa mikopo hiyo ili na wao waweze kupatiwa.

 

Alisema diwani huyo kupitia Chama Cha Mapinduzi kwamba katika kipindi cha mwaka mzima Kata ya Kindai ilikusanya jumla ya shilingi milioni 17 lakini pamoja na kiasi hicho kidogo walichokusanya,serikali kuu iliipatia kata hiyo shilingi bilioni 3.1 kwa ajili ya kukamilisha miradi mbali mbali ya maendeleo.

 

Hata hivyo diwani huyo kijana alitumia fursa hiyo kumshukuru Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania,Daktari Samia Suluhu Hassani kwa kuipatia kata hiyo jumla ya shilingi bilioni 3.1 zilizowawezesha kufanikisha miradi ya ujenzi wa shule,miundombinu ya barabara,ofisi za serikali za mitaa pamoja na kuviwezesha vikundi vya wajasiriamali mikopo kwa vikundi vya wanawake na vijana.

 

Naye diwani wa viti maalumu tarafa ya Mungumaji,Rehema Ntandu aliwasihi wale wote walioboresha taarifa zao kwenye daftari la kudumu la mpiga kura na wenye sifa za kupiga kura wajiandae kwenye uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika mwezi wa kumi mwaka huu

 

MWISHO.

Post a Comment

Previous Post Next Post