HALMASHAURI YA MANISPAA YA SINGIDA ITAENDELEA KUTEKELEZA ILANI YA UCHAGUZI KATIKA SEKTA YA MICHEZO

 

Na Jumbe Ismailly SINGIDA



HALMASHAURI ya Masispaa ya Singida itaendelea kutekeleza ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kwa kuwawezesha,kuwatia moyo pamoja na kuwahamasisha wananchi wa Manispaa ya Singida kushiriki katika michezo ili waweze kujiimarisha kiafya na kujikinga na magonjwa mbali mbali.

Akikabidhi zawadi kwa washindi wa mchezo wa bao wa kikundi cha mchezo wa bao cha Amani Singida Mjini,Meya wa Manispaa ya Singida,Yagi Maulidi Kiyaratu amesema kwamba michezo haina umri wala jinsia na ili kuukuza zaidi mchezo wa bao ameahidi kukiunganisha kikundi cha mchezo wa bao na wachezaji wa mchezo huo kwenye maeneo mengine ya Manispaa ya Singida ili waweze kuwa pamoja.

Kwa mujibu wa Yagi mchezo wa bao una historia kubwa hasa wakati wa kupata uhuru wa Tanzania kwani muasisi wa taifa hili marehemu Mwalimu Julius Kambarage Nyerere alikuwa akipenda sana kwenda kucheza bao na wazee ili kupata fursa ya kuongea nao,kuteka busara zao,kushauriana na hata wakati mwingine kushawishiana namna nzuri ya kuelekea kupata uhuru.

Hata hivyo Mstahiki Meya huyo ameweka bayana kwamba suala la michezo lipo kwenye ilani ya uchaguzi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) ya mwaka 2020-2025 kwenye eneo la michezo kwani katika ilani hiyo michezo ni kwa wote bila kujali umri,jinsia rangi wala dini ya mwanamichezo husika.

Muandaaji wa mashindano ya kutafuta walimbwende Mkoani wa Singida aliyeshiriki mchezo wa bao,Aunt Bora Lemmy ametumia fursa hiyo kuwatahadharisha wanawake wengine wanaokwepa kushiriki mchezo wa bao kwa kuamini kwamba mchezo huo ni wa wanaume peke yao,kuondokana na dhana hiyo  potofu na badala yake wajenge utamaduni wa kuamini mchezo huo ni kwa wote bila kujali umri,jinsia,dini na wala kabila la mshiriki..

Akitoa taarifa ya mashindano hayo ya mchezo wa bao,katibu wa kikundi  cha mchezo wa bao cha Amani Singida Mjini,Dr.Philip Kitundu amefafanua kuwa kati ya timu 17 zilizoshiriki mashindano hayo,timu nne za mwisho zimeshushwa daraja na hazitacheza ligi katika msimu ujao, na badala yake zitatakiwa kucheza michezo ya play off (championship),timu mbili zitakazoshinda zitarudi tena katika ligi kuu na zitakazoshindwa hazitashiriki kwenye mashindano msimu ujao.

Katibu huyo amewataja washindi wa mchezo huo wa bao kuwa ni pamoja na Dragoni Ramadhani aliyeshika nafasi ya kwanza kwa kuwa na alama 38, mshindi wa pili ni Omari Abrahamani aliyepata alama 35 na mshindi wa tatu ni Chief Sisco Ng;eni aliyepata alama 33.

MWISHO.

Post a Comment

Previous Post Next Post